BRAZIL VS CROATIA: HAKUNA KULALA LEO

Rio de Janeiro, Brazil
WENYEJI Brazil leo Alhamisi watakuwa na kibarua pevu cha kuhakikisha wanaanza vyema michuano ya Kombe la Dunia ambapo wanatarajiwa kufungua pazia kwa kumenyana na timu ya taifa ya Croatia kwenye  Uwanja wa Rio de Janeiro mjini hapa.
Ikumbukwe kuwa Croatia inayonolewa na Niko Kovač, haijawahi kuifunga Brazil zaidi ya kuambulia sare na vipigo hivyo leo inatarajiwa kuwa mechi ya kukata na shoka inayotarajiwa kuanza mishale ya saa 5 usiku.
Mara ya mwisho timu hizo zilipokutana kwenye michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2006 iliyofanyika nchini Ujerumani, Brazil  iliichapa Croatia bao 1-0 lililotupiwa kimiani na kiungo Ricardo Kaka ambaye mwaka huu hajaitwa katika timu hiyo.
Tayari mshambuliaji tegemeo wa Brazil, Neymar dos Santos, amesharejea uwanjani na ameahidi kufanya makubwa kwenye mechi ya leo.
Kwa upande wa Croatia kupitia kwa kocha wao Niko amesema kikosi chake hakitapaki basi kwenye mchezo wa leo ambao wenyeji wanapewa nafasi kubwa ya kushinda.  
Wachezaji tegemeo Brazil: Neymar, David Luiz, Dani Alves, Fred, Ramires, Paulinho, Marcelo, Willian, Hulk, Dante, Thiago Silva na kipa Julio Cesar.
Wachezaji tegemeo Croatia: Darijo Srna, Dejan Lovren, Vedran Corluka,  Danijel Pranjic, Luka Modric,  Mario Mandzukic, Ivica Olic, Eduardo
Previous
Next Post »

Blogger templates